+255 222215701   info@mloganzila.or.tz



Mloganzila yafanya upasuaji wa kuondoa uvimbe kwenye ubongo kwa kupitia pua.

Nov 9 2022

Timu ya wataalamu Bingwa wa Upasuaji Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu kwa kushirikiana na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Pua, Koo na Masikio (wa kwanza kulia) Dkt. Edwin Liyombo, akifuatiwa na Dkt. Alvin Miranda pamoja na Dkt. Raymond Makundi wakifanya upasuaji mkubwa wa kuondoa uvimbe kwenye sakafu ya ubongo kupitia pua bila kupasua fuvu la kichwa.

Daktari Bingwa wa Upasuaji Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu kutoka Marekani Prof. Dilantha Ellegala (wa kwanza kulia) akishirikiana na wataalamu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila kufanya upasuaji huo.

Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa Muhimbili, Prof. Mohamed Janabi akizungumza na waandishi wa habari kuelezea juu ya upasuaji huo.

Prof. Janabi akiwa katika picha ya pamoja na timu ya wataalamu walioshiriki upasuaji wa kuondoa uvimbe kwenye sakafu ya ubongo kupitia pua bila kupasua fuvu la kichwa.

Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila kwa mara ya kwanza imefanya upasuaji mkubwa wa kuondoa uvimbe kwenye sakafu ya ubongo kupitia pua (Endoscopic transphenoidal pituitary) bila kupasua fuvu la kichwa.

Upasuaji huu umefanywa na Madaktari Bingwa wa Upasuaji Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila pamoja na Prof. Dilantha Ellegala kutoka Marekani kwa kushirikiana na wataalamu Bingwa wa Magonjwa ya Pua, Koo na Masikio.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof. Mohamed Janabi amesema Hospitali ya Mloganzila ni ya pili kwa Hospitali za Umma hapa nchini kufanya upasuaji huu wa kibobezi.

Prof. Janabi ameishukuru serikali kwa kufanya uwekezaji mkubwa wa kuboresha sekta ya afya na kuwezesha huduma za kibobezi kutolewa nchini badala ya kupeleka wagonjwa kutibiwa nje ya nchi na kwamba upasuaji huu umefanikiwa kwasababu hospitali ina vifaa vya kisasa pamoja na wataalamu.

“Hapa imekuwa bora zaidi kwa mgonjwa huyu kwasababu tuna nafasi kubwa ya kufanya mazoezi, kuna nafasi kubwa ICU bila kuwa na msongamano mkubwa, rai yetu wananchi waendelee kuiamini hospitali yetu, tutaendelea kufanya oparesheni kubwa kama hizi katika hospitali zetu zote mbili Upanga na Mloganzila”amesema Prof. Janabi.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila Dkt. Japhet Ngerageza amesema matatizo ya uvimbe kwenye sakafu ya ubongo yanafika asilimia 10 hadi 15 ya matatizo yote ya uvimbe kwenye ubongo.

“Ni fursa kwa hospitali kwenda na mabadiliko ya teknolojia kwa kufanya upasuaji wa namna hii, juhudi zilizofanywa na hospitali tumeweza kuwa na timu yote ya wataalamu na kufanikiwa kufanya matibabu haya kupitia njia hii kwa mara ya kwanza katika hospitali yetu” amesema Dkt. Ngerageza.

Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Pua, Koo na Masikio kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt. Edwin Liyombo amesema awali upasuaji huu ulikua ukifanyika kwa kufungua fuvu ila kutokana na mabadiliko ya teknolojia sasa unafanyika kwa kupitia pua na kusisitiza kuwa upasuaji huu umefanyika na kupata matokeo mazuri.

Aidha Daktari Bingwa wa Upasuaji Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu kutoka Marekani, Prof. Dilantha Ellegala ameahidi kuendelea kushirikiana na Hospitali ya Taifa Muhimbili katika kubadilishana utaalamu na kupanua huduma za kibobezi ili kuzifanya ziwe endelevu katika Hospitali za Umma.